Tuesday, January 20, 2015

Wanalilia mali za wageni kuliko vifo vya wananchi!




PICHA ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, iliyochapishwa hivi karibuni kwenye vyombo vya habari ikimuonesha akilia mbele ya mali za mwekezaji zilizoharibiwa na wafugaji sikuipenda.

Kwenye Kaya yangu hasa eneo analotawala mkuu huyo wa mkoa kumekuwa na matukio mengi  ya mauaji ya wananchi yanayosababishwa na mgogoro wa ardhi baina ya wawekezaji, serikali na wafungaji; sote tunajua!
Hakiyamungu  sijawahi kumuona mkuu huyo wa mkoa akilia mbele ya maiti ya mfugaji hata mmoja. Nilichokiona juzi nilistaabu na kujiuliza kulikoni mkuu mwenzangu alilie mali za mwekezaji kuliko uhai wa wananchi anaowaongoza?
Mambo yako wazi; mgogoro kati ya Kampuni ya Kitalii ya Tanganyika Film Safary iliyochomewa mali zilizomliza mkuu wa mkoa dhidi ya wafugaji wa Kijiji cha Miti Mirefu wilayani Siha, Gama anaujua, lakini fikra kuwa ameshawahi kulia kuutatua haipo.
Kiongozi wa wafugaji wa Miti Mirefu, Kitasho Simeli amenukuliwa mara kadhaa akilalamika wachungaji kupigwa risasi na askari wa wanyamapori na maiti zao kutelekezwa porini bila serikali kuchukua hatua jambo linalochangia wananchi kuingiwa na hasira.
Hii ndiyo aina ya wakuu nilionao kwenye Kaya yangu, wanapolalamika wananchi wazalendo kufanyiwa unyama na hao tunaowaita wawekezaji hakuna kiongozi anayekuwa mkali; wanamaslahi binafsi sijui. Cha kujiuliza kwa nini walilie mali na siyo uhai wa watu?
Maana tungekuwa na uchungu na maisha tungelinda zaidi uhai wa watu kuliko mali. Mwekezaji anapoharibiwa mali zake si jambo la kumfanya mtu atoe machozi na kuacha kufanya hivyo anapoona maiti zimesambaa msituni huku kisa kikitajwa kuwa ni mgogoro wa ardhi.
Nimpe taarifa Gama na viongozi wengine wa kaya hii, mali anazozililia zina mbadala wake, mhusika atalipwa bima na fidia nyingine na maisha yataendelea, lakini uhai wa watu utarejeshwa kwa njia gani? Fikra pevu zinahitajika kujua hili.
Hatuwezi kuwa na taifa lenye viongozi wanaolilia mali na kuacha kulilia uhai ambao ni haki ya kikatiba ya wananchi. Hatuwezi kuwa na wakuu wanaoumizwa zaidi na uharibifu wa mali za wageni zaidi ya mali za wazawa. Hatuwezi pia kujenga taifa lenye usawa kama tutathamini mali za wawekezaji zaidi ya mali za wananchi wetu.
Tunawezaje kusema tunawatumikia wananchi kwa usawa kama hatuumizwi na vifo vya ng’ombe wao wanaokosa malisho wanayoyadai kila mara bila kuwapatia ufumbuzi madai yao na wakati huohuo tukaonesha upendeleo wa wazi kwa wageni?
Mkuu wa Kaya siwezi kukubaliana na hali hii kwamba niwaache wakuu wa mikoa walilie mali za wawekezaji na wasifanye hivyo kwenye vifo vya ng’ombe wa wafugaji ambao kwa tafsiri yetu hiyo ni pia ni mali sawa na magari ya Tanganyika Film Safary yaliyochomwa moto.
Ni lazima mimi kama Mkuu wa Kaya nisimamie mageuzi ya ufahamu, niongoze mfumo mpya wa kuongoza wananchi kwenye kaya hii ili mambo yasiendelee kwenda mrama.
Miaka nenda rudi migogoro ya wakulima na wafugaji inaendelea, watu wanakufa kila mahali katika kaya hii, mwitio wenye utashi kwa viongozi haupo!
Hivi tunashindwaje kutenga maeneo ya malisho na kilimo kwenye nchi kubwa kama hii? Hii ni aibu ya viongozi.
Ni ugumu gani uliopo wa kumaliza tofauti kati ya wawekezaji na wafugaji hasa kwenye maeneo ya hifadhi tulizozitengea sheria za kitalii. Hili halitutoi machozi ila tukiona mali ambazo siyo zetu majozi waaaaa! Ni aibu kubwa!

No comments:

Post a Comment