Tuesday, January 20, 2015

MNAWAFELISHA WAWE MAHAUSIGELI NA MAHAUSIBOI WENU




ENZI za mkoloni ambazo Mkuu wa Kaya nilikuwepo; mpango mahususi ulikuwa  elimu bora ni kwa watu weupe.
Weusi hawapekuwa nafasi kwenye shule bora kwa kuwa mkakati uliwataka waendelee kuwa mbumbumbu ili wawe watumwa katika mashamba ya mkonge na katani.

Shukrani ukombozi ukaja, Rais wa Tanganyika Huru, Julius Nyerere akafuta kikwazo hicho. Mwaka 1964 ukaanzishwa mpango wa elimu bora kwa wote, lengo likiwa ni kuwaelimisha wazawa wapate uwezo wa kujitawala.
Kwa kiasi fulani hilo lilifanikiwa. Wakati mwingine nikiwasikia hawa wazeewazee wanaojifanya wajuaji kwenye kaya yangu huwa nawaangalia halafu nacheeeeeka,  kwa sababu najua wao hawakutengwa katika elimu enzi za utoto na ujana wao lakini bila aibu siku hizi kwa kupewa vivyeo uchwara wanawasahau watoto wa wakulima.
Leo ukienda shule za kata humkuti mtoto wa mkuu wa mkoa wala wa katibu tawala, wote wanasoma shule za akademi zinazofundisha kwa kimombo. Ukiwahoji kulikoni ninyi viongozi mjitengenezee ka-utaratibu ka-ubaguzi? Wanakujibu, shule za kata hazitoi elimu bora, ujinga kabisa! Kama  hazitoi elimu bora uongozi wao kwenye kaya hii una faida gani? Hasiraaa!!
Hivi mwenzao naye (Nyerere) angefanya kama wanavyofanya nchi hii, wao si wangekuwa walima nyanya tu? Kwani alikuwa na shida gani kuwasaidia wapate elimu bora wakati leo wanashindwa hata kumuenzi!
Lakini kwa kuwa aliwaza ukombozi, alifikiri zaidi ya familia yake, alikuwa muumini wa mafanikio ya wengine alianzisha elimu bora kwa wote; matokeo ambayo yameleta matunda ya watu wasomi wengi wanaolisaidia taifa kwa namna fulani kipindi hiki.
Swali; ninyi viongozi mnashindwa nini kuifanya elimu ya nchi hii kuwa bora kwa kila mtu? Ukiangalia takwimu za ufaulu wa darasa la saba mwaka huu utangundua kuwa karibu nusu ya wanafunzi tena wenye umri mdogo wamefeli, ukimuuliza waziri mwenye dhamana; hao wanafunzi waliofeli anawapeleka wapi kupata elimu maana siyo ombi ni haki yao ya kikatiba, ‘atachekacheka’ tu!
Ukimuuliza wanafunzi wa kidato cha nne waliofeli mwaka jana serikali yake chini ya wizara yake imewaandalia mazingira gani ya kujielimisha, imewawekea mkakati gani wa kuondokana na ukosefu wa ajira, amewapangia utaratibu upi wa kujielimisha ili waendane na kasi ya ulimwengu wa sayansi na teknolojia? Huwezi kupata jibu la uhakika ni kuchekacheka tu.
 Wakoloni hawakupenda kuwasomesha wazawa kwa sababu walitaka watumwa wa kuwafanyisha kazi ngumu. Je, huu mpango wa serikali wa kutowajali wanafunzi zaidi ya nusu wanaofeli kila mwaka umejikita katika kujiandalia mahausigeli na mahausiboi katika nyumba za viongozi na mashamba ya watoto wa wakubwa wa nchi hii?
Kama sivyo kwa nini hakuna mipango thabiti ya kuwapatia elimu? Ukiiangalia elimu ya leo imejaa upendeleo kila mahali; inawezekanaje wanafunzi wanaosoma vijijini kusikokuwa na maabara, umeme, wala shule za awali wakashindanishwa mtihani mmoja na wanafunzi wanaosoma shule za akademi?
Mimi kama Mkuu wa Kaya naziona kasoro hizi katika kaya yangu na wananzengo wenzangu kwa nini mawaziri wanaolipwa mishahara na marupurupu makubwa akili zao haziwafikishi kwenye kiwango hiki cha utambuzi?
Naona kwa utaratibu huu wa kutowasaidia wanaofeli zaidi ya nusu kwa miaka 20 ijayo taifa litakuwa na mbumbumbu zaidi ya nusu ambao hawatakuwa na sifa ya kuendana na kasi ya ulimwengu wa sayansi na hivyo kulirudisha taifa hili katika utumwa wa fikra alioupinga Nyerere.
Hivi inashindikana nini kujipanga kuhakikisha kuwa elimu katika kaya yetu inakuwa bora kwa kila Mtanzania? Tuliwachoka wakoloni tukawaondoa madarakani bila shaka tutawachoka watawala wavivu wa kufikiri na kuwaondoa.

No comments:

Post a Comment