Friday, April 18, 2014

Kwa nini wengine wanafanikiwa na wengine hawafanikiwi?



NI imani yangu kuwa, si wote wanaofahamu kwamba duniani kuna makundi manne ya watu wanaotafuta mafanikio, jambo linalochangia kwa kiasi kikubwa kuwafanya wakose majibu ya kwa nini hawa wafanikiwe kimaisha na wengine wasifanikiwe kabisa.

Kwa kufahamu hilo, nimeona ni vyema nikaandika makala haya kuhusu aina za watu katika ulimwengu wa mafanikio ili kuamsha akili za watu katika kukabiliana na changamoto nyingi za kimaisha.

Katika ulimwengu wa mafanikio binadamu wamegawanyika katika makundi manne ambayo ni WATENDA USAHIHI, WANAOLIDHIKA, WANAOTAKA KUPENDWA NA WASHINDI.

WATENDA USAHIHI:
 Ni watu ambao katika maisha yao huwa hawataki kukosea au kuonekana wayafanyayo si sahihi. Watu wa aina hii huwa ni wagumu sana kufanya jambo ambalo akili zao hazihakiki kuwa litamalizika kwa mafanikio.

Kikwazo kikubwa kwa watu wa aina hii mara nyingi ni kusitasita katika kuamuzi. Ni watu wa kuogopa macho ya watu hasa suala la kushindwa kutimiza malengo linapowajia akilini. Kinachowaogopesha zaidi watu wa kundi hili ni kuaibika mbele za watu jambo fulani likiwaharibikia.

WANAOLIDHIKA:
 Kundi jingine la watu katika ulimwengu wa mafanikio ni wale wanaolidhishwa na hali zao na kwamba hawahitaji mabadiliko ya aina yoyote kwenye maisha yao.
 “Ndugu yangu, hali hii tumeizoea, mwaka wa nne huu.” Wamezoea maisha magumu na hawataki kujituma kutafuta.
Hata hivyo, wapo wanaozoea kazi na majukumu yao ya kila siku kiasi kwamba hawataki kubadilika, hawapendi kuongezeka zaidi ya hapo walipo. Utakuta uwezo wa mfanyakazi alioanza nao miaka 7 iliyopita ni huohuo mpaka leo.

Wafanyakazi wengine wanaweza kuajiriliwa nyuma yake wakajitahidi kusoma, kujifunza kazi na kupanda vyeo na kumwacha mlidhikaji yuko palepale. Kundi la wanaolidhika.

WANAOTAKA KUPENDWA:
 Kuna watu katika maisha yao wanataka kumfurahisha kila mtu kwa lengo la kuvuta upendo wa wanadamu wenzao. 

Asilimia kubwa ya kipato chao hukitumia kwa lengo la kuwatumikia ndugu na marafiki, kuwasaidia katika shida zao na kujikuta wakisahau kufanya mambo yao ya kimaendeleo.

WASHINDI: 
Kundi la mwisho la watu ni wale ambao katika maisha yao ya kila siku hupenda kufika kwenye kilele cha mambo yote wanayofanya.
Hutamani kufanikiwa zaidi na zaidi, hawakubali jambo liwashinde, kila walichokusudia kukifanya huakikisha kwamba wanakabiliana na changamoto zote na mwisho wa safari kupata ushindi.

Baada ya kuangalia hayo, ni vema kujiuliza; Je ni sahihi kutokuwa makini katika mambo yako ama kulidhika na mafanikio uliyoyapata? Je ni sahihi mtu kuacha kuwasadia wenzake kwa hofu ya kuwa katika kundi la tatu? 

Jibu ni hili: Ni vema mambo matatu  ya mwanzo yakaongozwa na la nne yaani USHINDI. Kwa maana hiyo kila mmoja wetu lazima awe mtu ambaye anatamani sana kufanikiwa katika maisha yake ya kila siku. 
Watu wote wakiwa na nia hii wataweza kuyapita makundi mengine matatu kwa uangalizi mkubwa.
Hawatakubali wawe makini wasifikie malengo, hawataacha kujaribu bahati kwenye mambo ambayo akili zinaona ni magumu, hawatalidhishwa na mafanikio au hali walizonazo na hawatakubali kutumika kama wafurahisha watu bali kwa kila kitu watafanya kwa kiasi kwa lengo la kufika katika mafanikio sahihi.

No comments:

Post a Comment