Friday, May 21, 2010

Wanawake huishi umri mrefu zaidi ya wanaume



Inaweza ikawa ni mada ngumu kuikubali kutokana na sababu kadha wa kadha, lakini ukweli unabaki kuwa wanawake wamebainika kuwa na uwezo wa kuishi miaka mingi zaidi ya wanaume, hii ni kwa mujibu wa tafiti nyingi zilizofanywa hivi karibuni ulimwengu, ukiwemo ule ulioendeshwa na wanasayansi wa Chuo cha Liverpool John Moores (LJMU) nchini Uingereza.

Profesa David Goldspink wa LJMU anayejihusisha zaidi na seli za binadamu alieleza matokeo ya utafiti wa jopo lake kuwa “tumebaini kwamba nguvu za moyo wa mwanaume hupungua kwa asilimia 20 – 25 kutoka miaka 18 hadi 70, lakini nguvu ya mioyo ya wanawake wenye umri wa miaka 70 haitofautiani na ya vijana wenye umri wa miaka 20.”

Kwa maana hiyo mwanaume kadili anavyozidi kupata umri mkubwa, nguvu za moyo wake hushuka na hivyo kupunguza kiwango cha msukumo wa damu mwilini na kusababisha madhara ya kiafya na hatimaye kifo. Lakini kwa mujibu wa utafiti huo huo ambao ulihusisha zaidi ya wanawake na wanaume wenye afya 250, ulibaini kuwa mioyo ya wazee wa kike huwa haipunguwi nguvu kutokana na umri wao.

Ifahamike kuwa ukimchukua mwanamke mwenye umri wa miaka 20 ukampima msukumo wa moyo wake ukalinganisha na mzee wa miaka 80 utapata nguvu sawa. Kibaiolojia ni kwamba wanawake wameumbwa tofauti na wanaume, ndiyo maana wanatajwa kuishi miaka 5-13 zaidi ya wanaume na kwamba kiwango hiki kimekuwa kikiongezaeka kutoka karne moja hadi nyingine.


Mazingira ambayo yanashibisha hoja hii ni pamoja na mfumo mzima wa masuala ya kujamiina ambayo huwahusisha watu wa jinsia mbili tofauti. Hata ukiangalia utofauti ulioanishwa mara nyingi na watafiti umewashirikisha zaidi wanawake wenye umri kati ya miaka 18 na kuendeleza, umri ambao kwa kawaida wasichana wengi huwa tayari wamevunja ungo na wengine kuanza kushiriki tendo la ndoa.

Randolph Nesse, mwanasaikolojia wa Marekani aliwahi kueleza faida anazopata mwanamke wakati wa tendo la ndoa na kipindi cha siku zake ambazo zinatajwa pia kumsaidia katika kusafisha kemikali za mwili wake na kwamba upo ushihidi kuwa mwanamke asipoingia kwenye siku zake afya yake huyumba.

Maelezo haya na mengine yahusuyo mwanamume kutoa mbegu wakati wa tendo la ndoa yanaweza kuwa sababu ya kuweza kutofautisha umri wa kuishi kati ya mwanaume na mwanamke na kuzidi kuweka hatari kubwa ya umri wa wanaume kuendelea kupungua kama elimu ya kujihami na tatizo hili haitatolewa kwa wahusika.

Kumekuwa na hoja nyingi kuhusu tatizo la wanaume kupungukiwa na umri wa kuishi, wapo wanaosema kuwa wingi wa majukumu ya kifamilia huwapunguzia umri wanaume, hata hivyo njia pekee zinazotajwa kuwasidia mwanaume kuweza kuimarisha mapigo ya moyo wake ni hizi zifuatazo:

KWANZA- Ili mwanaume aweze kuusaidia moyo wake kuwa na nguvu katika kipindi chake cha maisha ni lazima afanye mazoezi ya mwili. Wanaume wengi wamekuwa wakipuuza ufanyaji wa mazoezi, jambo ambalo ni hatari kwa afya zao. Ufanyaji wa mazoezi unaweza kuusadia mwili wa mwanaume kuongeza msukumo wa damu na kumuwezesha kutoa kemikali hatari mwilini kwa njia ya jasho ambalo haliwezi kutoka kama mtu atakuwa amekaa na kuendekeza starehe.

PILI- Mwanaume anashauri kupunguza kiwango cha kufanyaji mapenzi. Upunguzaji huu utasaidia kuufanya mwili wake uwe na seli za kutosha kulingana na lishe anayopata, hata hivyo kama mwanaume anataka kufanya mapenzi kwa kiwango cha mara tatu au nne kwa siku lazima azingatie mlo wenye nguvu. Lakini kwa wanaume ambao ni dhaifu, wakiwemo wenye virusi vya UKIMWI hawashauriwi kufanya ngono mara kwa mara.

TATU- Kucha kutunza hasira kifuani. Wanawake wengi hufanikiwa kupumzisha miili yao kwa sababu ni wepesi wa kukasika na kumaliza mambo tofauti na wanaume ambao hutajwa kutumia muda mwingi kufuga chuki moyoni. Inashauriwa kuwa kama kuna jambo ambalo limetokea ni vema kulimaliza na kuachana nalo, ili kuufanya mwili uwe huru. Kitendo cha kuweka hasira mwilini huchangia moyo kupungukiwa na nguvu za kufanya kazi sawa sawa.

NNE – Kuzingatia lishe bora, kupata muda wa kupumzisha mwili, kuepuka matumizi ya kemikali kama pombe kali na vinywaji vyenye nikotini pamoja na kupata vipimo vya kitabibu hasa vya moyo kila baada ya miezi mitatu ili kufahamu mapema matatizo ya moyo wake na kuweza kuyatibu mapema.

Pamoja na ukweli kwamba wanawake wanaishi umri mkubwa zaidi ya wanaume, Daktari Carol . J . Hogue wa Marekani anawashauri wanawake wote kuzingatia afya ya uzazi salama, anaseme miongoni mwa mambo ambayo yanawapunguzia umri wa kuishi wanawake ni pamoja na suala la uzazi. Anasema ili mwanamke aweze kuishi zaidi ya mwanaume ni vema akapanga uzazi. Inaelezwa kuwa kipindi cha mwanamke kujifungua ndicho kinachotajwa kuhatarisha maisha ya wanawake wengi.

Makala haya yanazingatia ukweli wa vifo vitokanavyo na hitilafu za udhaifu wa mwili si ajali na majanga mengine kwamba wenye hatari ya kufariki dunia ni wanaume peke yao.

No comments:

Post a Comment