Friday, May 21, 2010

Unaweza kupunguza uwezekano wa kufa mapema kwa kucheka



Habari za leo mpenzi msomaji wangu na heri ya mwaka mpya 2008. Leo nimekuja na somo zuri ambalo nalitoa kama zawadi ya mwaka huu kwako. Kama wengi wetu tujuavyo, kiwango cha miaka ya kuishi hasa katika nchi za ulimwengu wa tatu kimepungua sana nyakati hizi, hivyo kila tunaposherekea mwaka mpya tunasherekea pia uzee na utimilifu wa miaka yatu ya kufa, lakini hilo lisitupe hofu kwani wataalam wamegundua maajabu yapatikanayo kwa mtu kucheka.

Kwa kutambua umuhimu wa maajabu hayo nimeona ni vema nikaelezea faida za mtu kucheka. Ifahamike kuwa watafiti mbalimbali duniani wamebaini kuwa mtu anaweza kujikinga, kujiponya na magonjwa hatari ya kansa, moyo na kisukari kwa kucheka na isitoshe achekaye anatajwa kuufanya mwili wake usionekane umezeeka hata kama atakuwa na umri mkubwa.
Kwa mujibu wa watafiti wa masuala ya kijamii, ugumu wa maisha unaoleta msongo wa mawazo ndiyo unaotajwa kuchangia vifo vya wanadamu wengi sambamba na kufupisha umri wa kuishi. Wanasema mtu mwenye kutingwa na sononi kila mara huchoma seli nyingi muhimu katika mwili wake, hivyo kumfanya awe katika hatari ya kushambuliwa na magonjwa niliyoyataja hapo juu.
Katika tafiti za hivi karibuni ukiwemo ule uliyoendeshwa na wasomi wa Chuo Kikuu cha Amerika Cardiology, imebainika kuwa uhaba wa furaha hasa fursa ya watu kupata muda wa kucheka kwa siku ni moja kati ya sababu kubwa zinazochangia magonjwa hatari miongoni mwa watu wengi. Wanasema watu wengi wamechipusha vimelea vya magonjwa si kutokana na bakteria halisi bali mfadhaiko wa mioyo yao.
Kwa maana hiyo wataalam hao wameibuka na ushauri kuwa ni bora watu wakajibidisha kutafuta furaha katika maisha yao kuliko kudumu katika uhangaikia tiba ghali za dawa zinazotolewa na vituo vya afya na hospitali, ilhali mzizi wa magonjwa yao unatokana na wao wenyewe kuishi bila kicheko ambacho kinatafsiri furaha aliyonayo mtu husika (kumbuka sizungumzii kicheko cha kebehi).
Kwa mujibu wa wasomi hao imegundulika kuwa kicheko ni tiba na kinga bora ya magonjwa yanayomkabili mwanadamu yakiwemo magonjwa ya moyo ambayo ni hatari sana kwa uhai. Mtu ambaye anaweza kutumia dakika 20 kwa siku kwa kucheka, anaweza kutibu maradhi yake hata bila kumeza vidonge. Inatajwa kuwa kicheko huweza kukuza mara dufu uzalishaji wa 'Immuni' ambazo ndizo zenye kazi ya kuukinga mwili usishambuliwe na bakteria.
Kwa maana hiyo, mwili wa mtu ambaye anaishi kwa kucheka kwa kiwango hicho nilichokitaja unaelezwa na wataalam hao kuwa, utakuwa na uwezo wa ajabu wa kuua na kusisafisha kemikali za hatari zinazozalishwa mwilini. Kama hilo halitoshi, upo pia uwezo wa kuzalisha kiwango sahihi cha sukari kwa mwili wa mtu mwenye furaha inayoambatana na kucheka mara kwa mara.
Uzoefu uliopatikana kutoka katika Hospitali ya watoto ya Manchester nchini Marekani ambayo hutumia katuni na filamu za kuchekesha kwa wagonjwa wanaolazwa hapo, umebaini kuwa kuna kiwango kikubwa cha nafuu wanachopata wagojwa hata kabla ya kuanza kwa tiba za magonjwa yanayowakabili.
Kutokana na faida zinazopatikana kutokana na kucheka ikiwemo hiyo tiba ya ajabu ya magonjwa, Dr Madan Kataria wa India mwaka 1998 aliitangaza Mei 6 ya kila mwaka iwe ni siku ya kicheko duniani, ambapo zaidi ya nchi 50 zilikubali kuiadhimisha, ikiwa kama ishara ya kumuunga mkono Dr Madan katika hamasa yake ya kujenga familia, urafiki na ujamaa wenye furaha.
Kwa mantiki hiyo ni jambo la busara kwa kila mtu ndani ya familia na sehemu za kazi kutafuta uhusiano wenye furaha, ili uweze kuchochea kicheko ambacho ni muhimu sana katika maisha ya mwandamu. Lakini kinachoshangaza na ambacho kimetajwa pia na wataalam hao ni kuwa watu wengi siku hizi wanaishi maisha yaliyo mbali na furaha jambo ambalo ni hatari kwa afya.
Inasikitisha kuona kwamba kadili miaka inavyosonga mbele familia nyingi zimekuwa na maisha ya yaliyojaa kununiana na kutofurahishana. Si ajabu mtu akawa ni mwenye kukunja uso tangu asubuhi mpaka jioni kiasi cha kutoona maana ya kukaa na kufurahi na wenzake ndani ya nyumba. Ifahamike kuwa mtu wa tabia hiyo anakuwa katika mazingira ya hatari ya kufariki mapema (utafiti sio hali halisi) au kuonekana mzee ilhali umri wake ni mdogo.
Kwa kuzingatia hayo mimi pia natoa ushauri wangu kuwa kila mmoja wetu ajitahidi kubadili mfumo wa maisha yake kwa mwaka huu kutoka katika mifarakano inayoondoa furaha katika jamii na kutafuta kuishi kwa furaha inayotajwa kuwa na faida katika afya zetu. Mbali na hilo tunaweza kujikuta tunatafuta pesa na hatimaye kushindwa kuzitumia kwa raha kutokana na kuandamwa na magonjwa ambayo tunaweza kuyaepuka kwa kujifurahisha wenyewe.
Hatuna budi pia kwa mwaka huu kila mmoja wetu kuhakikisha kuwa anakuwa na jukumu la kumsaidia jirani au rafiki yake ili awe mbali na msongo wa mawazo. Hata pale inapopatikana fursa ya kwenda kuwaona wagonjwa tunatakiwa kuwatazama huku tukionesha tabasamu na kuwatia moyo. Kinyume chake tukienda kuwatazama kwa huzuni na maneno ya kusikitisha tunawaongezea hofu na matokeo yake ni kuwazidishia maumivu.

No comments:

Post a Comment