Tuesday, April 13, 2010

HASARA ZA KUPENDA KUPITA KIASI




Kupenda ni jambo muhimu katika maisha ya mwanadamu, kwa sababu asilimia kubwa ya matendo ya mtu huongozwa na mapenzi. Miongoni mwetu kuna watu wanapenda waume/wake zao, mali, watoto, magari vyakula, vinywaji, michezo na pengine aina fulani ya maisha.

Baadhi yetu tuko tayari kupoteza maisha kama tutaachwa na wapenzi au kukosa mambo tuliyoyapenda. Pamoja na kwamba moyo hupata maumivu pale mazuri yanapokosekana, bado kuna ukweli juu ya madhara ya kujitakia yanayoweza kuepukwa na mtu anayeumia kwa kiwango cha kukosa usinginzi, kulia mara kwa mara kiasi cha kushindwa kufanya kazi zake kama kawaida.

Kupenda kwa kiwango cha kushindwa kujizuia na kuvumilia ni hatari kwa afya ya mwanadamu, kwani uchunguzi unaonesha kuwa watu wengi wanaosumbuliwa na ugonjwa wa vidonda vya tumbo, moyo na wale wenye magonjwa yasiyoonekana kitalaamu pamoja na wanaokufa ghafla ni athari za msongo wa mawazo utokanao na kukosa mazuri wanayohitaji katika maisha yao.(Jiulize ni kipi kinachokutia simanzi moyoni mwako).

Kisaikolojia kuutesa moyo kwa sababu mpenzi wako kakukataa ni matokeo ya kufikiri vibaya kwani ushahidi uliopo miongoni mwetu unaonesha kuwa mapenzi si kitu cha kudumu kwa miaka mingi na anayesema anaweza kupenda jambo moja milele kwa kiwango kilekile ni mtu anayejiwekea mtengo utakaomnasa mwenyewe na kumtesa.

Watu wengi tunaowaona wakipagawa baada ya kupewa talaka na waume zao au kuondolewa mambo fulani waliyokuwa wanayapenda ni wale walioyachukulia mapenzi kama kitu cha kudumu kisichoweza kubadilika, huku wakisahau ukweli kuwa wanayopenda kwa wakati huo hawakuzaliwa nayo na wala hawakuyapenda kabla.

Licha ya kuwepo kwa umuhimu wa kujiaminisha katika kupenda kwa msingi wa muda mrefu, mtu hatakiwi kukataa mabadiliko yanapotokea kwani ni wazi kwamba tuliyopenda tulipokuwa watoto si yale tunayopenda sasa. Hivyo ni jukumu la kila mtu anayetaka kuwa salama na maumivu ya moyo ya kumkosa ampendaye ni kuwa tayari kubadilika kutoka kupenda kitu cha awali mpaka kijacho, kuliko kung’ang’ania wazo moja na kujitesa nalo.

Historia ya mafanikio ya watu inaonesha kuwa waliokuwa tayari kuacha walivyovipenda na kuanza mambo mapya ndiyo waliofanikiwa. Mwalimu wangu na bosi wangu Eric Shigongo aliwahi kuniambia kuwa alilazimika kuondoka nyumbani kwao Mwanza,akaacha aliowapenda/alivyovipenda kuja Dar es Salaam kutafuta maisha, leo hii ni miongoni mwa waliopiga hatua.
Katika hali ya kawaida ni vigumu sana kuondoka miongoni mwa watu uliowazoea, kuacha makazi yako na kuhamia mkoa mwingine, kuachana na mpenzi wako mliyeahidiana mambo mengi, lakini mafanikio na usalama wa maisha unataka mtu awe jasiri wa kupokea changamoto zinazohusu mapenzi.
Ikiwa umekaa na mwanaume kwa muda mrefu na ukabaini kuwa hana mtazamo wa kimaendeleo, uwe tayari kukubali mabadiko ya kumwacha na kuanza maisha mapya.

Msomaji wangu, unaumia kwa sababu mpenzi wako ameamua kuachana na wewe na sasa unafikiria kujiua, hebu kaa chini ufikirie kabla ya kuwa na huyo maisha yalikuwa hayaendi? Kama sivyo kinachokuumiza hasa ni nini mpaka unashinda unalia na kuutesa moyo wako?

Tambua kuwa dunia ina vitu vingi sana vya kupenda, ambavyo vimeumbwa kwa ajili ya mwanadamu, usipopenda hiki haina maana hakuna cha kukufaa kipo na asipokupenda ndugu yako wapo marafiki watakaochukua nafasi ya mapenzi moyoni mwako na maisha yatasonga mbele kwa mafanikio makubwa, unachotakiwa ni kujiamini.
Kwa elimu zaidi ya masuala ya maisha na mapenzi, msaada wa mbinu za kusoma na kufaulu mitihani nunua kitabu changu cha saikolojia na maisha.

2 comments:

  1. Ni sawa ulivyoeleza, japo ungekamilisha kwa kunukuu katika Biblia ama Kurahni if unaitumia. Ni vizuri kufanya maamuzi ya kuacha jambo ama mambo flani ili ufikie mafanikio. Lakini kuna mambo ambayo iwe iweje huruhusiwi kuacha. Kwa wakristo suala la kuacha mke uliefunga nae ndoa si halali kwa mujibu wa biblia maana ALIYEKIUNGANISHA MUNGU, MWANADAMU ASIKITENGANISHE.

    Issue inakuja hivi hasa watu wanapokuwa wamefikia hatua ya kuachana:

    Hatumhusishi Mungu wakati tunapochagua ni nani awe mwenzi. Ukweli uliopo kanuni ya Biblia ukiifuatilia kwa kina ina mantiki na Nguvu sana na hutendeka, tumia muda wako kufanya utafiti juu ya hili. Wasabato wanawafundisha vijana wao mbinu na namna ya kupata na kumchunguza mtu atakaye kuwa mwenzi, lakini je ni wote hufanikiwa?

    Tuna mitizamo na uelewa mfupi sana, kwa nini.
    Leo hii ukishauriwa usile sembe hutafurahi na kukubali, na akija mwingine akwakmbie ugali wa sembe ama dona usile kabisa ama ule kwa nadra sana bado ni vigumu hoja hii kueleweka.

    Kihistoria, watu weupe walibuni njia ya kuhafifisha uwezo wa kufikiri hasa kwa mwafrika hata kama atakuwa amesoma. Ugali ulibuniwa kudumaza ubongo, fuatilia uwezo wa kufikiri wa mwafrika linganisha na white people, zipo tofauti. Kusudi lao ni nini, rasilimali zilizopo Afrika zinawaumiza vichwa white people.

    Tunaweza ona aina ya ukarimu tunaoupata.
    Hili linatupatia picha kuwa kuna hasara ya kupenda kupita kiasi maana hata maadili kuporomoka chanzo chake ni kupenda tamaduni za kimagharibi kupita kiasi sababu ikiwa tunapenda TV na VIDEO MUSIC ama FILAMU za huko.

    Kuna kazi ya ziada ya kuelimisha.

    ReplyDelete
  2. nikweli ila hauna reference za kuonesha UGALI ULIBUNIWA LINI,WAPI NA NANI ALIYE BUNI.sio vizuri mtu mzima kusema uongo

    ReplyDelete