Tuesday, January 20, 2015

WANAFUNZI UDOM KUPIGWA MABOMU, SERIKALI ITAPIGWA NINI?



JESHI la polisi hivi karibuni lilisambaratisha maandamano ya wananafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (Udom) kwa mabomu, silaha za moto na matumizi ya nguvu kupita kiasi.

Kwa sababu ya amani ya nchi yangu siungi mkono machafuko, migomo na maandamano, jambo linalonifanya nisikemee moja kwa moja hatua iliyochukuliwa na polisi.
Pamoja na uzalendo huo, kasumba ya mkuki kwa nguruwe kwa binadamu mchungu inanikera sana, sana, sana! Sina mbadala wa kauli hii hata kama asiyeiabudu falsafa hii ni baba yangu mzazi.
Binafsi niliyashuhudia matumizi ya nguvu ya polisi katika kukabiliana na maandamamo hayo. Nasikitika kusema hata damu za wanafunzi niliona zikimwagika. Nikajiuliza chanzo cha tatizo ni nini? Mwanafunzi mmoja aliniambia:
“Tulipanga kwenda ofisi ya waziri mkuu kuonana naye ili tuwasilishe madai yetu, tumekuwepo chuoni kama watu tuliotelekezwa, hatuna chakula na fedha tulizoahidiwa kupewa hatujapewa, fedha za malazi na viandikwa nazo hakuna, sasa uwepo wetu shuleni una maana gani?”
Hii ndiyo hoja ya msingi iliyoandaa mgomo. Nyongeza ya madai ya kuongezewa posho ya chakula ilijumlishwa kwenye ajenda katika hali ya kufikisha hisia zinazowakwaza wanafunzi hao wa programu maalumu iliyoandaliwa na serikali kwa lengo la kuzalisha walimu.
Upembuzi; ni nani kati ya rais, waziri mkuu, waziri wa fedha na watendaji wa serikali, mwenye uwezo wa kufanya kazi bila kula? Shujaa gani anayeweza kutumika kwa moyo bila kuwa na mahali pa kulala na vitendea kazi?
Jibu hakuna; jambo ambalo linayafanya madai ya wanafunzi hao kuwa ya msingi yasiyoweza kumalizwa kwa majibu dhaifu ya: “Muwe wavumilivu.”  Mkuu wa idara anayesema wanafunzi wavumilie njaa yeye tumbo limejaa nyama choma na mvinyo!
Anayehimiza wenzake wavumilie hawezi kutembea kwa miguu hata hatua kumi. Anayehimiza uvumilivu hajawahi hata siku moja kulala njaa na isitoshe hajacheleweshewa malipo ya posho zake akavumilia lau kwa mwezi mmoja!
Hili ndilo jambo linalonisikitisha; serikali inawezaje kutumia nguvu kuwapiga mabomu na risasi watu ambao imeshindwa kuwatimizia ahadi zao?
Hoja ingejengwa kwamba, wanafunzi hawa wamelipwa kiasi fulani lakini bado wamekomaa kudai anasa zaidi, watu wangeelewa. Lakini kutumia silaha za moto kumwaga damu huku udhaifu ukiisuta serikali, haliwezi kuwa jambo linaloweza kuvumiliwa.
Nimesema mara nyingi, rais anaweza asiwe dhaifu, chama tawala kinaweza kisiwe cha mafisadi kama watu wanavyodai lakini baadhi ya watendaji wake hawawezi kukwepa lawama hizi! Na hawa ndiyo kansa ya ustawi wa jamii.
Nathibitisha; miaka miwili iliyopita baadhi ya watendaji wa bodi ya mikopo waliingia matatani baada ya kubainika kulipa mikopo hewa kwa wanafunzi. Mchezo huu siyo mgeni, kwa mpenda haki anaposikia fedha fulani za mkopo zimechelewa lazima ahoji mantiki yake. Maana siku hizi inadaiwa fedha hucheleweshwa wakati mwingine kwa sababu zinachezewa upatu.
Kibaya zaidi mamlaka za serikali zimekuwa kimya mno, ingekuwa sawa basi baada ya malalamiko ya wanafunzi juu ya maisha magumu chuoni, kutolewe ufafanuzi wa kina na pengine wanafunzi kwa kushirikiana na wakuu wa vyuo kukutana kutafuta suluhu ya uhakika ili maisha yaende.
Yote hayo hayafanyiki; badala yake serikali inasubiri watu wagome iamuru wapigwe risasi za miguu, huu siyo utawala bora hata kidogo.
Kinachoniumiza zaidi ni kwamba uhusiano baina ya serikali na wananchi unaharibika siku hadi siku hivyo kuifanya nchi kuwa katika hatari ya kuingia kwenye machafuko. Nachochea hivi;  serikali inayopiga mabomu raia wadai haki, yenyewe itapigwa na nini? Akili kichwani!

No comments:

Post a Comment