Thursday, January 22, 2015

UBAYA NI KIOO; UNAOUONA KWA WENZAKO NI WAKO



Watu wengi huhangaika sana kujua kama wanaifurahisha jamii au wanaiudhi. Wengine wamefikia hatua ya kujiuliza, wamekosea nini watu wanaowazunguka  mpaka wakajikuta wamechukiwa?  Kisaikolojia fikra za namna hii, ni  sawa na kutafuta gari kwenye mwanga kwa njia ya kupapasa!
“Nashanga mama mdogo ananichukia bure,  tena hakuna kosa nililomfanyia lakini hanipendi tu” Je wewe nawe umekuwa miongoni mwa watu wanaodhani unachukiwa bure?
Achana na hulka hiyo, hebu tambua ubaya wako kwa kuangalia vidokezo vifuatavyo, ambavyo naamini ukivisoma kwa umakini utagundua ni wapi unakosea hadi kufikia hatua ya kuchukiwa katika jamii.

Je, inapotokea umesababisha wenzako wajisikie vibaya huwa unajisikiaje moyoni mwako? Mfano ulikuwa katika mazungumzo ya kawaida na rafiki yako, lakini kwa sababu za kibinadamu akapokea mazungumzo yako vibaya na kufadhaika. Wewe unapotambua kuwa umemuondolea mwenzako furaha huwa unajisikiaje moyoni? Kama huumizwi na tukio hilo tambua kuwa wewe ni mtu mbaya.
Jiulize, katika maisha yako ni mara ngapi umewafanya wengine wafurahi kwa kuwatatulia matatizo yao, kuwasaidia katika shida na kuwavusha katika hali ngumu za kimaisha? Au umekuwa mtu wa kusubiri usaidiwe wewe hata kwa vitu unavyoweza kuwasaidia wenzako?
Tangu umeanza kazi umeshawahi kutoa sehemu ya mshahara/pato lako kuwasaidia wazazi na ndugu zako au umekuwa mtu wa kutoa visingizio vya hali ngumu ya maisha licha ya kuwa unafanya anasa mjini? Ikiwa hujawahi kuwasaidia watu kupata furaha, fahamu kuwa unaishi na ubaya kwenye jamii,  jiandae kuchukiwa.
Je, unaposikia wenzako wana shida huwa unazichukuliaje?, je ni sehemu ya tatizo lako au hujiweka pembeni na kuwaachia binadamu wenzako wamalize matatizo yao? Ukiwa hivyo hicho ni kipimo kikubwa cha ubaya wako kwenye jamii unayoishi.
Umekuwa ukitumiaje uwezo wako  wa mali au hata nguvu za mwili mbele ya wenzako? Je, ni kwa kuonea na kuwakandamiza watu  uliowazidi? Ikiwa una tabia hiyo anza kujihesabu kuanzia leo kwamba wewe ni mtu mbaya mbele ya jamii.
Angalia mazungumzo yako, je yamekuwa ni ya kuwatia moyo watu, kuwafariji na kuwaelimisha au umekuwa mtu wa kutoa matamshi ya kudhalilisha, kuudhi na kuwavunjia heshima wenzako? Kama ulimi wako unatoa maneno yenye ‘sumu’ usitegemee kupendwa.
Je umekuwa mtu wa haki, mwenye kuwatanguliza wenzako? Unaweza kutoa unachokitegemea ili kumsaidia binadamu mwenzio? Ukiwa huwezi kufanya hivyo na umekuwa mtu wa kukumbatia mali zako ujue wewe ni mbaya.
Toka ndani ya moyo wako unafurahia jamii kuwa na umoja au umekuwa mtu unayechochea migawanyiko baina ya watu wanaopendana? Endapo una tabia kama hiyo fahamu kuwa matendo yako ni mabaya.
Ni mara ngapi umezuia hasira zako kwa lengo la kuepusha migogoro? Unaweza kuvumilia kuonewa au umekuwa mtu wa kulipa kisasi kwa kudhamilia kufanya mambo mabaya kwa makusudi licha ya moyo wako kukuonya mara nyingi usifanye hivyo? Kama una tabia hiyo tambua kuwa huo ndiyo ubaya wako kwenye jamii, chukua hatua za kujisahihisha wewe kwanza kabla ya kuwanyooshea wenzako kidole!

No comments:

Post a Comment