Wednesday, January 14, 2015

HAYA NDIYO MAMBO YANAYOWEZA KUKUVUNJIA HESHIMA



HAKUNA kitu kibaya maishani kama kuonekana upo katika daraja la chini na mtu wa kudharaulika kwenye jamii unayoishi. Kisaikolojia kuna madhara makubwa.

Ni imani yangu kuwa kila mwanadamu timamu anapenda kuheshimiwa lakini wengi wetu tunashindwa kupata heshima tunayoitaka kwa sababu hatufahamu jinsi ya kuishi mbele ya wenzetu.

Kitaalamu, hakuna jambo ambalo hutokea maishani bila sababu maalumu hivyo hata kudharauliwa kwako au kwetu ndani ya jamii tunayoishi kunatokana na jinsi tunavyoenenda.
Mwalimu wangu wa somo la maisha na saikolojia, Eric Shigongo, aliwahi kuniambia ‘Nothing happens in the sky, but the elements should be there,’  akimaanisha kuwa hakuna kitokeacho angani pasipo kuwa na dalili au sababu zake.
Naomba nianze kutoa njia za kukusaidia kurejesha heshima yako kwa kuperuzi na wewe baadhi ya dokezo muhimu zinazoweza kukusaidia kujitambua na kuweza kuyaepuka maisha ya kudharauliwa.

MUONEKANO
Kwanza kabisa ni jinsi unavyoonekana. Muonekano ninaouzungumzia hapa ni usafi wa mavazi na mwili kwa ujumla. Hata siku moja hakuna mchafu anayeheshimika katika jamii anayoishi hata kama ana kipaji kikubwa kiasi gani.
Kwa hiyo uchafu wa mavazi na mwili huchangia mtu kudharauliwa katika jamii anayoishi. Linaweza kuwa jambo dogo sana lakini ni moja kati ya sababu kubwa inayochangia kuporomoka kwa thamani yako mbele ya wenzako.

Mazungumzo
Hapa naomba nieleweke kuwa unachokizungumza kinaweza kukujengea heshima au kukubomolea heshima. Kauli zisizo na busara zitakufanya udharaulike kwa kila mtu. Uropokaji usiokuwa na mantiki huchangia kuporomosha heshima yako hasa kama utakuwa muongeaji zaidi. Biblia inasema penye wingi wa maneno hapakosi uovu.

UTENDAKAZI WAKO
Ndugu zangu, siku zote heshima ya mtu ni kazi. Watu wengi hawapendi kufanya kazi kwa bidii huku wengine wakijiendekeza kwa tabia ya kuombaomba, jambo hilo halifai kwa vile huchangia kubomoa heshima yako mbele ya jamii. Fanya kazi usiishi bila kujishughulisha.

KUTOTIMIZA AHADI
Kama una tabia za kuahidi mambo halafu unashindwa kuyatekeleza, basi unajiweka katika nafasi mbaya ya kutunza heshima yako katika jamii unayoishi. Bora ukwepe kutoa ahadi kuliko kuahidi na kutotimiza.

SIFA ZISIZO NA MAANA
Nakumbuka msemo mmoja kutoka kwa mwandishi mwandamizi aliyekuwa mtaalamu wa falsafa za maisha, marehemu Adolf Balingilaki, ambao unasema kwamba:
“Ukitafuta heshima kwa gharama ya juu, basi utalipwa dharau kwa bei nafuu.”
Msemo huu unamaanisha nini? Siku zote ukiwa unafanya mambo yako kwa ajili ya kusifiwa au mazungumzo yako kuwa ya kujiinua, watu watakudharau.

KUTOKUWA MWAMINIFU
Suala la uaminifu ni pana, kuna uaminifu wa fedha, siri, dhamana na mambo kama hayo, hivyo ni vema kila unachoaminiwa lazima ukitunze kwani ukiwa mtu wa kuvunja uaminifu fahamu kuwa utashusha heshima yako.

No comments:

Post a Comment