Wednesday, May 19, 2010

Huu ni msaada pekee kwa watu wenye ufahamu mdogo




Kama wewe ni mmoja kati ya watu ambao wana tatizo la ufahamu mdogo au mwanao ungana nami upate ufumbuzi wa tatizo hili.Uchunguzi unaonyesha kuwa shuleni, kazini na kwenye jamii kuna watu ambao wanadharaulika kwa sababu si wazima katika uelewa. Hali hii imekuwa ikiwauma wahusika hasa pale wanapojaribu kufanya mambo kwa uwezo wao wote na kupata matokeo dhaifu.

Wanafunzi wengi wamejaribu kusoma kwa bidii, lakini wamejikuta katika nafasi za chini, wengine wametumia uwezo wao katika kazi, lakini ukaguzi wa bosi hukosoa walichofanya. Kwa kifupi watu wenye kasoro hii wamejikuta wakipoteza dhamana mbele ya wenzao. Kutwa hubebeshwa kauli hizi: “usimtume fulani hataweza” “Somo gani, la Kiswahili? Hawezi.” “Hana uwezo wa kuoa.”

Kauli hizi zinauma na wengi zimewakatisha tamaa. Wazazi wamewatenga watoto wao kwa sababu wanashindwa kupata alama za juu katika mitihani yao. “Wewe shule huwezi labda usubiri kuolewa” Mtoto huyu hasara tupu haelewi kabisa unapomwambia” Lakini je saikolojia inaamini katika kushindwa? Jibu ni hapana kwa sababu historia inaonyesha kuna watu wengi ambao walikuwa hawawezi lakini baadaye waliweza. Njia ya kufanya ni hii!


JUKUMU LA MHUSIKA
Jukumu la mhusika katika kushughulikia tatizo la ufahamu mdogo ni kujitambua. Atambue maeneo ambayo yanamkwaza na ayaorozeshe tayari kwa kuyaongezea umakini.Kama ni masomo basi ajue ni yepi yanamshinda, kama ni yote uchungu wake usiwe kuona aibu baada ya kudharauliwa bali kwa kushindwa kufanikiwa.

Mhusika atenge muda wa kutosha kujizoeza katika yale anayofundishwa na awe na wakati wa kuyarudia. Aepuke kuchanganya mambo kabla ya kutimiza alichokusudia kukifanya. Mbio zake ziwe ni kupata alichokilenga. Kwa wale ambao ufahamu wao ni mdogo kazini nao vivyo hivyo wanatakiwa kujifunza kwa bidii na kuwaweka wenzao wanaoweza kama shabaha ya ukamilifu. Kujielimisha kupitia vyombo vya habari kusoma vitabu na kuwakaribu na wa wenye uelewa mkubwa ni jambo la muhimu.

Mwisho wahusika wanatakiwa kuwa mbali na hali ya kukata tamaa, hasa pale wanapojaribu jambo na kujikuta wamekosea. Wawe karibu zaidi na waalimu wao, wawe tayari kukiri kushindwa kwa lengo la kutaka msaada na kuepuka ukimya na kufanya jambo huku wakiwa na hofu au uelewa mdogo.


JUKUMU LA JAMII

Jukumu la jamii kwa watu kama hawa ni kuwatia moyo na kuepuka kutumia maneno ya kuwakatisha tamaa. Kwa mfano huwezi, utafeli, utaabika na kadhalika. Wajibu mwingine kwao ni kuwaongoza na kuwasaidia kwa upole, kuwa jamaa wapole wasiokejeli kasoro za rafiki, ndugu na watoto wao.

Wazazi wenye watoto wenye ufahamu mdogo wanajukumu la kuwasimamia na kuhakikisha wanatambua upungufu wao kisha kutafuta watalaamu au shule zenye sifa ya ufundishaji mzuri. Kazini nako wakuu wanatakiwa kuwaamini wafanyakazi wao na kuwatia moyo, hata wanapokosea, wasiwakalipie kupita kiasi.

JUKUMU LA TAIFA
Taifa kwa maana ya serikali ina wajibu wa kufanya utafiti ambao utachanganua mazingira, jamii na mahitaji ili kujua wapi pana hitaji msaada zaidi na wa aina gani. Kwa mfano, dunia nzima leo watu wanatumia kompyuta, lakini hapa nchini kuna idadi kubwa ya wanafunzi au watu wazima makazini ambao hawajawahi hata kuiona. Kwa maana hiyo wau hawa wanabaki kuwa na ufahamu mdogo wa mambo si kwa makosa yao bali mazingira wanayoishi.

Sasa unaweza kupata msaada wa mawazo juu ya matatizo yako ya kimaisha kwa kuwasiliana nami. Uliza chochote kuhusu mambo ya ndoa na mapenzi, mfadhaiko wa moyo, mikwamo ya kimaisha, kuacha ulevi, sigara pamoja na jinsi ya kutatua migogoro ya kifamilia. Bila shaka utajibiwa ndani ya gazeti hili au moja kwa moja.

No comments:

Post a Comment