Wednesday, April 7, 2010

MAMBO YA KUHUZUNISHA NA NAMNA YA KUYAKABILI




KUFIWA NA MUME/MKE

Jambo la kwanza linalohuzunisha zaidi ambalo lina kiwango cha asilimia 100 ni mtu kufiwa na mke au mume. Rekodi zinaonesha kuwa, watu wanaofiwa na wapenzi wao huwa na huzuni kubwa kiasi cha kutishia maisha yao.

Msongo wa mawazo, mauzauza ni mambo ambayo yanatajwa kusababisha vifo vya ghafla na vya muda mfupi kwa watu waliofiwa na waume/wake zao, huku sababu ya vifo hivyo ikibaki kuwa ni msongo wa mawazo (stress).
Licha ya ukweli kwamba kufiwa mume/mke ni jambo zito lakini, huzuni inapokuwa ya kudumu kiasi cha kutishia maisha ya mtu, suala la uzembe wa kufikiri huchukua nafasi.

Hivyo, ili mtu aweze kuepukana na matatizo yanayotokana na kufiwa ni lazima afuate muongozo ufuatao ambao utamsaidia kuipunguza au kuiondoa huzuni hiyo ambayo ni mbaya kuliko nyingine zote duniani.

Kwanza, ni kukubaliana na ukweli kwamba mwenza amefariki na hatarudi, kulia na kuhuzunika hakusaidii. Pili ni kuziondoa taratibu kumbukumbu zote zinazokuja na kutawala mawazo kuhusu mkeo/mumeo aliyekufa.

Usiyazamishe mawazo kwenye tukio hilo, ukiona kuwaza kunajitokeza ni bora kupuuza mawazo hayo kwa kutoyapa nafasi ya kukutawala. Usipende kukaa peke yako kwa muda mrefu. Usiangalie picha na kutembelea kaburi la marehemu mara kwa mara bila kuwa na sababu za msingi.

Usivute taswira ya maisha mliyokuwa mkiishi zamani. Kaa karibu na watu uwapendao, tembelea sehemu zenye kuvutia. Epuka kuzungumzia mambo ya marehemu wako. Badili mazingira ya chumba mlichokuwa mkilala, kuwa bize na majukumu yako na andaa mipango ya kumtafuta mwenza mpya.



TALAKA

Suala la kutalikiana linahuzunisha watu kwa asilimia 73, wengi kati ya wanaokumbwa na kadhia hii wanatajwa kuwa ni wanawake, ambao kwa nchi za dunia ya tatu ndiyo wanaoondolewa kwenye himaya zao za ndoa kwa vile wanaume ni watumwa wa mfumo dume. Hata hivyo imebainika kuwa wanaoumia zaidi ni wale wanaoachwa bila kuwa na makosa ya msingi (haibagui wanaume au wanawake).

Mwanamke au mwanaume aliyetendwa, hukumbwa na msongo wa mawazo, hasa anapofikiria sababu dhaifu za kuachwa kwake na pengine kulinganisha kuachwa na wema aliomtendea mwenzake wakati wakiishi pamoja. Kwa mujibu wa uchunguzi, watu wanaohangaika na mawazo ya kuachwa ni wale wanaodhani wamedhalilika (Inferiority complex) kwa kuachwa kwao. Mara nyingi huwa ni watu wa kutojiamini juu ya kuweza kuishi maisha ya upweke na wakati mwingine kudhani jamii inawacheka.

Ifahamike kwamba kuachana si kashfa, mtu anayeachwa anatakiwa kujiamini na kuishi kwa wema ili kuiaminisha jamii kuhusu tabia yake njema na kuwafanya watu waone kuwa mhusika hakustahili kuachwa.
Aliyeachwa lazima ajitume kufanya kazi kwa bidii na apange mipango yake mipya ya kimaisha, lengo likiwa ni kuonesha uwezo wake wa kuishi peke yake. Asijenge chuki kwa mwenzake, asipange kulipa kisasi aepuke kuchunguza mwenendo wa mwenziwe, kukutana au kuwasiliana naye. Aishi karibu na rafiki, watoto au ndugu zake, awapende na aombe ushauri kwao mahali anapoona anakwama, azuie mawazo ya kuachwa.

MIGOGORO YA NDOA

Watu ambao hawaishi kwa amani kwenye ndoa zao ni wepesi wa kupatwa na msongo wa mawazo. Ndoa zenye wanaume/ wanawake wasaliti zinahuzunisha wengi. Lakini ushauri wa kitaalamu unaotolewa kuhusu jambo hili ni kila mwanandoa kumtambua mwenzake kitabia na anapoona hakuna ulinganifu amchukulie mwenzie kama mgonjwa mwenye kuhitaji tiba na wala si mtesaji.

Haifai kumfumania mwezako na kuanza kuwaza na kulia badala ya kutafuta ufumbuzi au kwa lugha nyingine tiba. Ni vema kila tatizo limalizwe kwa mwafaka, kasoro za mume au mke zisihifadhiwe kifuani na kupewa muda wa kuumiza akili.

Viongozi wa dini, ndugu, wazee, rafiki, wanaweza kusaidia kujenga nyufa za ndoa. Pale inapothibitika kwa ushahidi kuwa mwanaume/mwanamke hawezi kujirekebisha hakuna njia salama ya muumizwaji zaidi ya kuvunja ndoa au uhusiano wake na huyo mwanaume/mwanamke. Haipendezi kuzidisha kiwango cha uvumilivu kwa vile madhara yake huwa ni makubwa.

KUFUNGWA JELA

Maisha ya gerezani yanaumiza. Wafungwa wengi hasa wa magereza yaliyopo ulimwengu wa tatu, hali za wafungwa huwa ni mbaya. Wengi hufariki kifungoni au muda mfupi baada ya kumaliza. Hii inatokana na magonjwa ambayo hutokea kwa sababu ya kushindwa kumudu mazingira na wakati mwingine kutokukabiliana na matokeo ya hukumu, jambo ambalo huwafanya wafungwa wengi kuwa na sononi zisizo isha. Hivyo ili kukabiliana na huzuni ya kufungwa lazima mfungwa mwenyewe akubaliane kwanza na matokeo.

Jambo la pili ni kuacha kushindana na mshtaki wako kwa kutumia akili, usikaribishe mjadala wa mawazo kwenye akili yako, chukulia kwamba hiyo ni bahati mbaya ya maisha yako sawa na ajali. Hesabu kuwa hayo ni mapito na ipo siku utatoka ukiwa mshindi na ukweli utajulikana.

Nelson Mandela alipofungwa alituliza mawazo na hatimaye alitoka na kuwa rais wa nchi na leo ukweli wa kuonewa kwake kila mtu kaufahamu. Ushauri mwingine ni kuzidisha upendo kwa wenzako, kuwa mwema, ridhika na upatacho na wakati mwingine tumaini siku njema kwa kuiambia nafsi yako kuwa, maisha ya gerezani yatapita au kama kifungo ni cha maisha, huna budi kukubali kuishi kama mfungwa.

KIFO CHA NDUGU WA KARIBU
Anapofariki baba, mama, kaka, dada, mtoto wako huzuni hutamalaki. Lakini ni vema ukarejea sehemu ya kwanza kwa masaada zaidi. Ila kwa nyongeza usiwe mtu wa kulinganisha matokeo ya maisha yako ya uyatima na yale yaliyokuwepo wakati wazazi.

Kwa mfano usidhani unateseka kwa sababu wazazi wako hawapo (wamekufa), inawezekana hata wangekuwepo ungeteseka vile vile. Pambana na maisha wewe kama wewe hatimaye utashinda. Kumbuka kadiri unavyolia ndivyo unavyozidi kujitesa na kujisogeza kwenye hali mbaya na pengine kufa mapema.

Hebu fikiria wangapi wamefiwa na wazazi wao, lakini wanaishi leo maisha ya raha, kwa nini wewe usiweze. Au ni wangapi walifiwa na watoto na leo wamepata wengine wazuri.. Kumbuka kupenda kilichokufa ni kukinai kilicho hai na kutopenda kijacho. Hivyo kama unampenda zaidi mtoto aliyekufa sina shaka utamdharau uliyenaye na upo uwezekano hata usipate mwingine kwani mawazo yako yanaweza kuharibu afya yako na kukufanya usishike mimba maisha yako yote.

KUUGUA AU KUJERUHIWA

Watu wengi wanapojeruhiwa hasa vibaya au kupatwa na magonjwa sugu yanayotajwa kuwa hayana tiba hufadhaika sana. Mgonjwa kama kansa, kisukari, ukimwi, BP yamewahuzunisha wengi, hii inatokana na hofu ya kufa, ingawa ukweli unabaki kuwa kifo hakina ushirika na magonjwa hayo tu kwani kuna wanaokufa bila kuugua magonjwa hayo.

Jambo kubwa la kufanya ni kuondoa hofu kwa kuchukua mifano ya watu ambao wameishi/wanaishi kwa muda mrefu wakiwa na magonjwa hayo, lakini hawajafa. Usijifananishe na waliokufa mapema kwani inawezekana walikuwa na hofu ndiyo maana wakafa. Hofu ndiyo inayotajwa kuua watu wengi kuliko hata magonjwa yenyewe. Acha kufikiria mawazo ya kufa, usikate tamaa, endelea kufanya mambo yako kama kawaida na uwe karibu na watu wa kukufariji si wa kukuvunja moyo.

Usijihukumu kuwa ni mkosa mbele ya jamii na usione kama umeonewa na Mungu. Tembelea wagonjwa wengine hospitali, huko utaona wenye shida zaidi yako, hiyo itakupa unafuu wa kubeba udhaifu wako. Kwa wale waliopata ajali ni vema wakakubaliana na matokeo, wakatulia na kuwatembelea watu wenye ulemavu ili kupata msaada wa kimawazo na wakati mwingine kufanya ibada ya kuomba wapewe uvumilivu.

Ifahamike kuwa, ulimwenguni kuna walemavu wengi ambao wana maisha mazuri kuliko hata wazima, hivyo basi kuwa kilema haimaanishi kuwa umefikia mwisho wa maisha.


NDOA

Mazingira ya ndoa hasa yanapokuwa magumu tofauti na mategemeo ya awali hutia huzuni. Pesa inapokosekana, mke/mume anapokuwa haeleweki, ndugu na jamaa wanapokuwa na tabia mbaya zinazokwenda kinyume na misingi ya ndoa ni mambo yanayotia simanzi. Lakini pamoja na hayo kukosekana kwa mtoto ni jambo linalowafadhaisha watu wengi.

Namna ya kwanza ya kufanya ni kwa wanandoa wenyewe kuondoa mikwaruzano baina yao, hili likifanyika litawapa uwezo wa kukabiliana na matokeo yote mabaya na kupata ushindi, lakini pia wanandoa wanaopatana ni rahisi kufarijiana katika shida kuliko wenye migogoro.

Ni jukumu la wanandoa kukuza uhusiano na upendo ili kutiana moyo nyakati za shida. Kuepuka maneno ya kusikia na wakati mwingine kutozingatia kejeli za watu wa pembeni wanaobeza maisha yao ya ndoa. Kuwa na imani kwamba nyakati za kufanikiwa kwa kupata mtoto zipo na hakuna kukata tamaa kwa kuangalia muda mlioishi kwenye ndoa.

Lakini hata kwa wale ambao bado hawajaolewa nao wasihuzunike, kwani mara nyingi ndoa hutengenezwa na watu wenyewe kupitia wapenzi ambao uchunguzi unaonyesha kuwa asilimia kubwa ya wanaotaka ndoa wana wapenzi.

KUFUKUZWA KAZI

Watu wengi huchanganyikiwa au hushindwa kumudu maisha muda mfupi baada ya kufukuzwa kazi. Hii inatokana na vyanzo vya mapato kukoma na pengine heshima ndani ya jamii kupungua. Jambo kubwa la kufanya baada ya kutimuliwa kazi ni kutulia. Kama ilivyo kwa vifungu vingine ni vema mtu aliyefukuzwa kazi akawa karibu na marafiki sahihi ambao watamshauri na kumkutia moyo.

Aliyefukuzwa kazi hatakiwi kujifungia ndani na kuwaza. Jukumu la kwanza kabisa ni kupunguza matumizi, kutafuta vyanzo mbadala vya kuingiza kipato kama kufanya kazi za ‘party time’ na kadhalika.

Kuanza kutafua ajira mpya kwa kupitia watu wako wa karibu uliokuwa nao kazini ni jambo la muhimu. Usikimbilie kurudi kijijini, kwani huko unaweza usimudu mazingira ya kimaisha. Omba msaada kwa ndugu pale unapoona mkwamo. Acha anasa na ulevi kwani utakuingiza kwenye matumizi makubwa pesa yasiyostahili kwa wakati huo na wakati mwingine kukuharibu fikra.

Kuwa mwaminifu na usimweleze kila mtu shida zako. Epuka ushawishi wa kimakundi. Itafute furaha kila wakati kwa kusikiliza muziki ili kuifanya akili iwe imara katika kukupa majibu ya nini cha kufanya baada ya kufukuzwa kazi. Maisha yanawezekana pia bila ajira kwani kuna wengi wanaishi bila kazi za viwandani. Kama kuna mafao uliyopewa baada ya kuondolewa kazini ni vema ukayatumia vema, ili yakusaidie wakati ukitafuta ajira mpya.


SULUHU BAINA YA WANA NDOA

Wapenzi na hasa wanandoa wanapokosana na mmoja kati yao akawa hataki suluhu, yule anayekataliwa huingia katika msongo mkubwa wa mawazo. Mawazo hutawala juu ya kufikia makubaliano na yule aliyempenda, hangaiko la moyo hutikisa mwili kiasi cha kutoweza kula wala kulala, hatimaye mtu hupata ugonjwa wa moyo na baadaye kupoteza maisha.

Inashauri kuwa mkishahitilafiana na mpenzi wako, mtafute umuombe radhi, akikataa washirikishe ndugu au rafiki wa karibu anayesikilizwa na mpenzi wako ili akusaidie kutafuta suluhu. Wazazi na wazee ni budi wakapewa nafasi pia.

Unapoomba msamaha usilazimishe sana kusamehewa, kufanya hivyo kunaweza kumpa kiburi mpenzi wako na kukataa kukusamehe kwa kujua huna pa kwenda na kwamba kukuacha kwake kunakuumiza. Suluhu inapokosekana unatakiwa kutuliza mawazo kwa kuutumia muda wako wa mapenzi kufanya kazi zako za kukuingizia kipato.Pendelea kubadilishana mawazo na watu wengine hasa wenye mafanikio.

KUSTAAFU KAZI

Uchunguzi unaonyesha kuwa, watu wengi hufariki dunia muda mfupi baada ya kustaafu kazi, hii inatokana na wengi wao kushindwa kumudu mazingira mapya ya maisha nje ya ajira zao. Kasoro kubwa inayopatikana kwa watu wa aina hii ni maandalizi mabaya ya kuelekea kustaafu.

Angalia mada kuhusu maisha ya uzeeni iliyopo ndani ya kitabu hiki ili kufahamu namna ya kustaafu kazi bila madhara. Lakini ni vema mtu aliyestaafu akatafuta shughuli mbadala itakayomfanya awe ‘bize’, asijiingize kwenye starehe na matumizi makubwa ya pesa, asikurupuke kufanya biashara na kuanzisha miradi mpaka ashauriwe, apunguze matumizi ya familia ili asome upya mfumo wa maisha bila kutegemea mshahara.

KUUGUZA NDUGU

Ni wazi kuwa watu wanapouguza ndugu zao huwa na huzuni hasa wanapowaona jinsi wanavyohangaika na maumivu. Ni kweli, inatia simanzi pale unapomuona mjomba, shangazi, mama mkubwa au shemeji yako akiugua, lakini njia ya kukabiliana na huzuni hiyo ni kutopima kwa kina namna anavyojisikia mgonjwa wako.

Elekeza nguvu katika kumsaidia, kumpenda kila anapoonekana kuumia, kuwa naye karibu na kumfariji, usioneshe huzuni mbele ya mgonjwa kwani kufanya hivyo ni sawa na kumvunja moyo na kumfanya mgonjwa wako ajisikie vibaya zaidi. Mara nyingi njia sahihi ya kumuuguza mgonjwa si kumuonea huruma bali ni kumpa faraja na kuamini kuwa atapona.


UJAUZITO

Ujauzito nao unatajwa kuwatia huzuni baadhi ya wanawake wajawazito. Wanawake wengi huwa na hofu ya kujifungua salama. Njia sahihi ya kuepuka tatizo hili ni kwa mjamzito mwenyewe kukwepa upweke na afanye mazoezi. Asikaribishe hofu kwa mambo ya kusikia juu ya mwanamke fulani aliyekufa wakati akijifungua au kutumia muda mwingi kuwaza namna atakavyoukabili uchungu wa kuzaa na hata kuhofu kupatwa na kifafa cha mimba na kupoteza maisha.

Wanaume na ndugu hawatakiwi kuwaudhi wajawazito. Kusikiliza muziki, kuangalia sinema za kufurahisha ni muhimu kwa mjamzito ili kumuondolea hofu ya kujifungua. Mjamzito hatakiwi kupewa taarifa za mtu aliyekufa akijifungua au kuogopeshwa kwa maneno kupitia hali aliyonayo. Kwa mfano “hee, miguu inavimba hii ni hatari sana inawezekana ukapata presha wakati unajifungua” Maneno haya hayafai kumwambia mjamzito na kama ana dalili mbaya ni vema apelekwe kwenye tiba kuliko kutishwa.

MATATIZO YA KUJAMIIANA

Hitilafu katika mambo ya kujamiiana hutia huzuni pia. Wanaume wenye kasoro za kimaumbile na upungufu wa nguvu za kiume, wanawake wasiohisi tendo hukabiliwa na msogo wa mawazo. Njia pekee ya kukabiliana na matatizo haya ni kuwaona wataalamu.Haifai kuumia kwa kuwaza namna ya kuondokana na tatizo la kasoro za kufanya mapenzi wakati tiba ipo.

Jambo jingine ni kwa wapenzi kuwa wawazi pale hisia zinapokosekana. Ni lazima kusaidiana kwa kushauriana, haipendezi kuyafanya mapenzi kuwa kitu cha siri. Kama mwenzio hakutoshelezi, ni vema kuwekana wazi na kutafuta suluhu ya tatizo kwa kuwashirikisha wataalamu na baadhi ya wazee ambao kimsingi wanafahamu mambo mengi.

KUISHI NA FAMILIA MPYA

Inashauri kwamba mtu anapoingia kwenye familia mpya (akiolewa, akiishi na ndugu katika ukoo, baada ya wazazi wake kufariki dunia), hatakiwi kujihukumu, akwepe kutafsiri atendewayo kama mtu ambaye si ndugu, bali kwa kila jambo aone anafundishwa na afanye kila awezalo kufuata kanuni na mazingira mapya.

Mara nyingi kinachowahuzunisha watu wengi wanaoishi ndani ya familia mpya ni mawazo yao, ambayo huwashawishi kufikiri kila baya wanalofanyiwa basi linatokana na sababu ya ujane au uyatiwa wao, wasifahamu kuwa kukoseana ni sehemu ya maisha tu na kinacholeta maana mbaya ni mawazo ya mtu si tendo lenyewe.

Jambo la msingi zaidi kwa mtu anayeishi na familia mpya ni kuwa na nidhamu ya hali ya juu, ajitume katika kufanya majukumu yake ya kimaisha na awe tayari kubadili tabia sawa na walezi wanavyotaka.

MABADILIKO YA KIBIASHARA

Kushuka kwa biashara, kubadili maeneo na hofu za kufilisika ni mambo ambayo huwatia simanzi watu katika kufikiri. Inashauriwa kuwa mtu anayeendesha biashara akiona dalili za biashara yake kushuka anatakiwa atafute mshauri wa biashara ili apate muongozo mpya.

Hifai kubabaika na kuwaza bila kutafuta kasoro zinazoporomosha biashara yako. Ni vema kupitia mapato na kubuni mikakati mipya ya kujenga panapobomoka. Ushauri wa rafiki mzoefu wa kibiashara ni mzuri pia. Lakini kujifunza mbinu mpya na kukabiliana na changamoto za kibiashara kwa kusoma masoko upya ni jambo linalotakiwa kufanyiwa kazi na mfanyabiasha yeyote. Haifai kuishi na wasiwasi wa kufilisika, kwani kufanya hivyo kuna madhara makubwa kisaikolojia.



KUHAMA NCHI
Unapohama nchi ambayo imeendelea kiuchumi na kuhamia nchi maskini utafadhaika au unapoambiwa kuwa unakwenda kuishi nje ya nchi unaweza kuwa na huzuni kwa upande mmoja, kwa mfano kufikiria maisha mapya mbali na jamii uliyoizoea na mambo kama hayo. Unachotakiwa kufanya ni kutobabaika na badala yake unachotakiwa kufanya ni kujifunza tamaduni za huko na kuwa tayari kubadilika na wakati mwingine kuyakubali mabadiliko hayo kama hatua za maisha yako. Mwisho ni kuwatumia wenyeji wako kama dira na kujitahidi kuwazoea na kuwafanya rafiki na ndugu zako.

RAFIKI KUFARIKI
Fuata muongozo wa kipengele cha kwanza na cha tano katika kupata ufumbuzi wa tatizo hili la kufiwa na rafiki yako. Haifai kusononeka kupita kiasi kwa suala ambalo huwezi kubadili matokeo yake.

MABADILIKO KAZINI

Ukibadilishwa kazi kutoka kitengo kimoja kwenda kingine kunaweza kukuhuzunisha, lakini unachotakiwa kufanya ni kuonyesha uwezo wako kwa kufanya kazi kwa furaha bila kupunguza nguvu, maana inawezekana ulipopangiwa, bosi wako kaona wewe unafaa au pengine unajaribiwa katika safari ya kupandishwa cheo.

KUPINGWA NA MKEO/MUMEO

Unapopingwa katika maamuzi yako na mumeo au mkeo ambaye awali alikuwa hafanyi hivyo unatakiwa kujiangalia mwenyewe mahali ulipokosea na kuangalia hoja za mwezako kuliko kuumia moyoni kwa kudhani unadharauliwa. Fanya uchunguzi, kuwa na mazungumzo ya kina na mwenzi wako ujue sababu ili marekebisho yafanyike haraka.

KUKOPA MKOPO MKUBWA
Watu wengi hushawishika kirahisi kukopa pesa nyingi, lakini wanapopewa na kuanza kutafakari namna ya kulipa huingiwa na huzuni, hivyo inashauriwa kuwa kabla ya kukopa mkopaji lazima ashauriwe na watalaamu namna ya kuutumia mkopo huo, ili aweze kujiamini na kuwa makini na urejeshaji ambao ndiyo huwatia hofu wakopaji wengi.

UREJESHAJI MKOPO

Unapokuwa umekopa au kuweka reheni kitu chako na hatimaye tarehe za mwisho za kurejesha zikawa usoni pako wakati ukiwa huna kitu/pesa, unaweza kubabaika na kuhuzunika. Unachotakiwa kufanya ni kutazama namna ya kupata pesa za kurejesha hata kwa kuuza vitu vingine visivyokuwa na umuhimu mkubwa ili kukomboa ulichoweka reheni. Kuwashirikisha ndugu,rafiki na watalaamu wa masuala ya pesa wakiwemo wakopeshaji ni suala muhimu.

KUBADILISHWA MAJUKUMU YA KAZI
Watu wengi hupatwa na huzuni pale wanapobadilishiwa majukumu kazini ikiwemo kuhamishwa vitengo, huku hofu yao ikiwa katika mapato na kumudu majukumu mapya waliyopangiwa. Jambo kubwa linalotakiwa kwa mfanyakazi anayehamishwa kitengo ni kujiamini na kuendelea kufanya kazi kwa nguvu. Kitendo chochote cha kuvunjika moyo baada ya mabadiliko huweza kumfanya apoteze uwezo wa kufanya kazi na kujikuta anafanya kazi kwa kiwango cha chini na kuonekana hafai na hatimaye kufukuzwa kazi.

MTOTO KUONDOKA NYUMBANI

Wazazi wengi huhuzunika pale mtoto ambaye walikuwa wanaishi naye anapofikia uamuzi wa kuondoka kwa sababu za kikazi, kimasomo, kuolewa na hata kujitegemea. Kimsingi huzuni hii ni ya bure kwa vile kukua kwa mtoto ni pamoja na kufikia hatua hizo za kuachana na wazazi na kuishi kama mtu mzima.

Hivyo, wazazi wanachotakiwa kufanya si kuhuzunika bali ni kuhakikisha kuwa wanampatia mtoto wao silaha za kuwa salama huko aendako ili aweze kuwasaidia. Ikiwa mtoto anakwenda shule basi ni lazima wazazi wamuwezeshe kusoma kwa furaha na ikiwa anaanza maisha mapya msaada wa mawazo na elimu ya maisha mapya ni vema kumpatia.



MATATIZO YA KISHERIA
Watu wengi hukumbwa na huzuni pale wanapokabiliwa na maatizo ya kisheria, kwa mfano kesi na tuhuma mbalimbali. Hata hivyo uchunguzi unaonyesha kuwa, huzuni za kupita kiasi zimekuwa chanzo kikuu kinachowafanya watu washindwe kukabiliana na tatizo lililopo mbele yao, hii inatokana na nguvu za mwili na ufahamu kuharibiwa na msongo wa mawazo.

Kwa maana hiyo tunapokuwa na tatizo lolote la kisheria, jambo la kwanza kabisa ni kutulia na kutafakari njia za kumaliza tatizo hilo kwa ushindi. Tafakari hizo lazima ziambatane na namna ya kupatana na walalamikaji, kupata watetezi wa kesi na ushauri wa namna ya kuendesha kesi iliyojitokeza. Si busara kupaniki na kuamua mambo kwa jazba, kufanya hivyo kumewaponza wengi ambao walikuwa na nafasi ya kushinda matatizo, lakini walikwama kwa sababu walipoteza umakini kwa jazba.

KUKWAMA KWA MALENGO

Tunaposhindwa kufikia malengo yetu tuliyojiwekea, kwa mfano kufeli mitihani, kushindwa kuendelea na ujenzi au kufanya hiki na kile tulichokusudia, mara nyingi hutuingiza kwenye huzuni, lakini kanuni za mafanikio yoyote duniani zinaanzia katika mkwamo.

Hivyo basi tunapoona tumeshindwa kufikia lengo la kile tulichotaka kukifanya haimaanishi kuwa hatuwezi, bali tumepungukiwa nguvu ambazo lazima tuzitafute kutoka katika miili yetu kwa kutumia uwezo na uelewa wetu ambao ni mkubwa mara 1000 ya tunaotumia kila siku katika maisha yetu.

Unapokuwa umekwama katika kitu chochote, jiulize sababu kwanini umeshindwa. Baada ya kupata sababu hizo tafakari njia na mbinu mpya za kuelekea kwenye ushindi huku ukiamini kuwa mafanikio yanatokana na juhudi pamoja na kutorudia makosa yaliyoleta mkwamo. Haifai kukata tamaa, hata kama umekwama mara elfu moja.

Tunapokwama mara kwa mara ni vema tukawashirikisha watu katika kila jambo tunaloona kuwa linasumbua akili, ushirikishaji huo unaweza kutusaidia kupata uzoefu kutoka kwa wenzetu ambao pengine wamevuka vikwazo vikubwa tofauti na hivyo tunavyokabiliana navyo.
Jambo la mwisho la kuzingatia tunapoanza hatua mpya za kuelekea katika ushindi tusikubali kurudia kosa, kama kufeli kwako mtihani kulitokana na kutosoma kwa bidii, usirudie kosa hilo ongeza bidii za kusoma au kama umeshindwa kujenga nyumba kwa sababu ya kuwa na matumizi makubwa ya pesa usikubali kuendelea na matumizi hayo, badala yake jibane na utimize nia yako.

MKE KUANZA/KUACHISHWA KAZI

Inaelezwa katika uchunguzi wa kitaalamu kuwa wanaume wengi huhofia wake zao kuanza kazi, hii inatokana na wivu wa kimapenzi . Wanaume hudhani kuwa mke anapokwenda kuajiriwa atakuwa na nafasi kubwa ya kushawishiwa kuanzisha uhusiano mpya na wanaume wengine.

Lakini ukweli ni kwamba huzuni hii mara nyingi huwa ni ya bure na matokeo yake huzaa wivu ambao husambaratisha ndoa na uhusiano. Kitu cha msingi kinachotakiwa kufanywa na mwanaume ni kuwa karibu na mkewe kumjengea hali ya kujiamini na kumtimizia yote anayostahili kama mke, likiwemo tendo la ndoa na ukaribu ambao mara nyingi unatajwa kuwa tiba kubwa ya usaliti.

Aidha kwa wale ambao wake zao wanafukuzwa kazi, jambo la muhimu ni kutiana moyo na kushirikiana kwa ukaribu kutumia muda wa dhahabu kupata kazi. Hili linatakiwa kwenda sambamba na kujaliana wakati wote wa tatizo. Hali yoyote ya kumtenga na kumwacha mkiwa ni hatari kwa uhusiano.
Pamoja na hilo endapo kipato cha mwanamke kilikuwa ni sehemu ya matumizi ya nyumbani basi mume na mke wanawajibu wa kukaa pamoja na kupanga upya matumizi yao ili kuondoa pato ambalo lilikuwa linatumika kutoka katika mshahara wa mwanamke ambaye kafutwa kazi.


KUANZA/KUMALIZA SHULE

Wanafunzi wengi wanapopata nafasi ya kuanza shule kwa hatua yoyote ile hujawa na hofu ya kuweza kukabili mazingira mapya. Inashauriwa kuwa mwanafunzi anapokwenda kuanza shule lazima awe tayari kubadilika kufuatana na mazingira na asiwe mtu wa kuogopa changamoto atakazokutana nazo shule, suala hili limeelezewa kwa kina katika kipengele cha mwanafunzi na mazingira ya shule ambacho kipo ndani ya kitabu hiki.

Hata hivyo, wanafunzi ambao wanamaliza shule wanashauriwa kutohuzunishwa na hilo, badala yake wawe tayari kujifunza maisha kutoka kwa ndugu wanaoishi nao.

MAISHA KUBADILIKA

Hali ya maisha inapoporomoka huhuzunisha, lakini kinachotakiwa katika kukabili tatizo hili si huzuni bali kuwa tayari kutazama kilichochangia kushuka kwa maisha hayo na kukitafutia ufumbuzi wa haraka.

Hata hivyo, watu wengi wanaelezwa kuwa wamekuwa wahanga wa tatizo la kuporomoka kwa maisha kutokana na ubinafsi kwa kutokuwa tayari kubadilishana mawazo na watu wengine katika kupata ufumbuzi wa tatizo na kuhakiki mipango ya maisha yao. Utakuta mtu akipata pesa basi anaamua mwenyewe kuanza biashara bila hata kupata ushauri kutoka kwa watu, hili ni jambo baya.

Ifahamike kuwa kubadilika kwa hali ya maisha ni dalili ya kuwepo kwa makosa makubwa katika mipango ya kimaisha, hivyo basi kila mtu anayepatwa na tatizo hili anatakiwa kutafuta msaada wa mawazo kutoka kwa wataalamu au rafiki, ili apate mbinu za haraka za kujinasua, kwani kuhuzinika peke yake hakufai.

KURUDI KWENYE MAKAZI YA AWALI
Mtu anapokuwa amehama nyumbani na kwenda kuanzisha maisha yake sehemu nyingine na baadaye kushindwa na kurudi nyumbani kwa wazazi au maskani yake ya mwanzo humfanya ahuzunike, lakini kitakachokuwa kinamhuzunisha si kitendo hicho, bali ni hisia za kudhani kuwa atadharauliwa au kuchekwa na watu.
Hili linaweza kuwa kweli, lakini huzuni pekee haisaidii kuondoa tatizo, wakati mwingine mbinu za kijeshi zinaelekeza kuwa unaposhindwa kusonga mbele na ulipo pakiwa na hatari ya kifo hatua za kurudi nyuma hustahili kutumika.

Kurudi huku hakupewi maana ya kushindwa, bali kujipanga katika kushambulia kwa nguvu. Kwa maana hiyo mtu anaposhindwa kuishi peke yake na akabaini kuwa kuwepo kwake katika maisha mapya ni kifo, kurudi nyumbani si kosa, kinachotakiwa ni nia ya kujipanga kuelekea katika ushindi mpya.

USUMBUFU WA BOSI KAZINI
Usumbufu wa mabosi kazini umekuwa ukiwafanya watu wengi kufikia hatua ya kuacha kazi, kuhama vituo au kufanya kazi kwa kiwango cha chini. Hali hii huwapata zaidi wanawake ambao wanafanya kazi na mabosi wanaowataka kimapenzi. Usumbufu wa kutongozwa sambamba na kitisho cha kufukuzwa kazi umekuwa ni huzuni kubwa kwa wanawake wengi makazini.

Inaelezwa na wanawake niliokutana nao wakati wa matayarisho ya kitabu hiki kuwa, kutongozwa na bosi ni kero ambayo haikwepeki hasa pale hisia za kimapenzi zinapokuwa hazipo kwa mtu husika. Wengi kati ya wanawake hukiri kufanya mapenzi na mabosi wao si kwa sababu wanawapenda, lakini kwa lengo la kulinda kazi ambayo huwa hatarini pale maelewano na bosi yanapoyumba.

Kusema kweli uamuzi wa kuwa mtumwa wa mtu kwa sababu ya kazi ni aibu kwa binadamu ambaye ameumbwa na uwezo utashi na nguvu za kukabili matatizo. Njia pekee ya kukabiliana na tatizo hili, kwanza ni kuwajibika katika majukumu kama mfanyakazi na pili ni kujiamini na kujipenda.
Unapowajibika kama ipasavyo unakuwa na ulinzi wa kazi yako si tu kwa yule unayemfanyia kazi, bali hata kwako mwenyewe kwa vile utakuwa na hoja za kujitetea kisheria. Lakini pia kujiamini na kujipenda ndiyo nguzo ya kukulinda wewe na ushawishi usiokuwa na tija kwako. Mfanyakazi lazima awe na msimamo wake kuhusu kazi anayoitumikia, ili asiyumbishwe na kitisho cha kufukuzwa kazi, kwani ajira kwa wachapa kazi zipo nyingi katika ulimwengu.

Mwisho ni kujipenda. Yaani kuwa mwanadamu mwenye utashi na kutokuwa tayari kuuza utu kwa sababu ya kazi. Endapo bosi atakuja na sera za kutongozana kazini, lazima aambiwe uwazi kuwa hilo haliwezekani na yeye auone msimamo, akitambua hilo hataweza kuleta usumbufu ambao hatimaye utamkosesha yeye mfanyakazi na kumtia aibu katika jamii. Lakini kufuata hatua za kisheria ni jambo linalofaa pia.

KUHAMA MAKAZI
Kuhamia katika nyumba mpya kunatajwa kuwatia hofu pia baadhi ya watu, inaeleza kuwa asilimia 20 ya watu wanaohama makazi yao ya awali huhuzunika. Hii inatokana na hofu ya kumudu mazingira mapya.
Watu wengi hushindwa kulala ugenini na kujikuta wakipoteza furaha kwa kiwango fulani. Inashauriwa kuwa mtu kabla hajahamia katika mazingira mapya ni vema akazoea taratibu maeneo anayokwenda, kuwatambua majirani na kusoma tabia zao, lakini zaidi ya yote ni kufuata misingi yote ya ubinadamu na kujiamini.

KUBADILI DINI

Watu wamekuwa wakibadili dini kwa lengo la kutafuta amani katika maisha yao kupitia njia ya kumwamini Mungu, lakini uchunguzi unaonyesha kuwa wengi wao wamekuwa hawapati amani hiyo kutokana na mambo mawili ambayo ni migogoro ya kifamilia na namna ya kumudu amri za dini mpya.

Asilimia 18 ya watu wanaobadili dini huhuzunishwa na mabadiliko hayo kiasi cha kujutia uamuzi wao, huku idadi yao wakitajwa kurejea katika dini zao za awali au kutaka tamaa ya kiimani na hivyo kupata madhara ya kisaikolojia.
Hata hivyo sababu za kitaalamu zinazotajwa kuchangia ukosefu wa amani hiyo ni udhaifu katika maamuzi. Watu wanaobadili dini wengi wao wamekuwa wakifanya hivyo kwa sababu dhaifu ambazo hutokana na shinikizo la watu wengi wakiwemo wapenzi au tamaa ya kupata pesa na misaada ya kidini, jambo ambalo ni hatari.

Inashauriwa kuwa mtu anayetaka kubadili dini lazima aamue mwenyewe na awe na sababu za msingi zinazodumu si za kimapenzi wala ushawishi wa kipesa, lakini pia awe tayari kukabiliana na matokeo hasi ya uamuzi wake, likiwemo suala la kutengwa na ndugu ambao hawatafurahishwa na maamuzi yake.

Vivyo hivyo, ni busara kuelewa mapema sheria na amri za dini mpya kabla hujajiunga, hili litasaidia katika kupima uwezo wa kutumikia kikamilifu kama muumini. Lakini ikitokea umeshindwa kupata amani uliyotaka, hakuna ubaya kurejea ulipotoka kwa maana ya kujilinda na athari za msongo wa mawazo utakaoletwa na kadhia za dini mpya.

FAMILIA KUBWA

Wazazi na walezi ambao wana familia kubwa wametajwa kuwa ni watu wanaosumbuliwa sana na msongo wa mawazo kwa kiwango ha asilimia 15. Malezi ya familia kubwa ni magumu hivyo walezi wengi hufikia kuona kero na usumbufu mkubwa hasa nyakati ambazo mahitaji ya familia huwa makubwa kuliko kipato. Hivyo ili mtu aweze kuepukana na tatizo hili lazima ahakikishe kuwa anakuwa na familia ndogo ambayo atamudu kuitunza.

Lakini ikiwa ni lazima kuwa na familia kubwa basi ni vema elimu ya kubana matumizi na uzalishaji wa pamoja ikatolewa ili kumfanya kila mtu ndani ya familia awajibike katika kubeba mzigo.


Haifai kuwa na familia kubwa ambayo watu wake hawazalishi. Kama una watoto ambao wanaweza kulima, kufanya biashara, hakikisha unawaongoza katika shughuli hizo, usiwaache walale na kula bure. Wafanye watu wa nyumba yako kuwa msaada kwako pia katika kuendesha gurudumu la maisha.

3 comments:

  1. Bwana akupe nguvu.ww ni mshauri mzuri sana ambaye umenisaidia mpendwa.


    ReplyDelete
  2. Bwana akupe nguvu.ww ni mshauri mzuri sana ambaye umenisaidia mpendwa.


    ReplyDelete
    Replies
    1. Makala hii imenisaidia sana
      Nmefiwa na mume wangu

      Delete