Friday, April 1, 2011

Hisia nane hatari katika mapenzi



Miongoni mwa vitu vinavyochangia kuharibu uhusiano wa kimapenzi ni hisia. Wapenzi wengi wameachana kwa sababu si kwamba walithibitisha ubaya wa wenzao ila walijijaza wenyewe hisia mbaya na kujikuta wamepoteza thamani ya kupenda. Hebu angalia hisia nane hatari ili uzikimbie mapema kabla hazijakuharibia penzi lako.

1. NASALITIWA

Kuishi katika mapenzi huku ukiwa na fikra kwamba mwenza wako anakusaliti ni jambo baya kwa vile huathiri msukumo wa ndani wa kupenda. Matokeo yake utajikuta ukishindwa kutimiza wajibu wako kama mke/mume kwa sababu tu ya kuendekeza hisia mbaya. Acha kuhisi, tafuta ukweli.

2. TUTAACHANA
Kuna wapenzi ambao wanaishi na mawazo ya “ipo siku tutaachana”. Wanafanya hivyo eti kwa kutafsiri mwenendo usioridhisha wa mapenzi yao. Kusema kweli hili ni jambo baya kwani huondoa ari na kujenga ufa wa mapenzi. Huwafanya wapenzi kubakia na wazo moja tu, la kutafuta sehemu mbadala ya kwenda baada ya kuachana. Usiwaze kabisa kuachana hata kama mnagombana na mwenzako kila siku.

3. SIWEZI MAPENZI
Baadhi ya wapenzi huwa na hisia kwamba hawayawezi mapenzi. Hata kama hawajaambiwa chochote kuhusu kutowatosheleza wenza wao faragha hukimbilia kujihukumu. Hujaambiwa kama umecheza chini ya kiwango, hofu ya nini? Usiwaze hivyo, kama una lolote linalokufanya uwe na hofu muulize mwenzio.

4. NINA KASORO
Naamini mitaani wapo watu ambao huamini wana kasoro fulani ndiyo maana hawafikii viwango vya kupendwa kama wanavyovihitaji. “Yaani mimi ningekuwa kama fulani ningefurahi sana lakini ufupi wangu ndiyo tatizo.” Hizi ni hisia mbaya tu, kumbuka kuna wafupi wanapendwa ile mbaya. Jisahihishe na epuka kujishusha hadhi kwenye hisia zako.

5. NITAMUUA
Miongoni mwa hisia mbaya kabisa kwenye mapenzi ni kufikiria kumuua mwenzako kwa sababu yoyote. “Nikimfumania na mwanaume mwingine nitamuua.” Mtu anayetawaliwa na mawazo ya aina hii anajiweka katika mtego mbaya kisaikolojia wa kuja kutekeleza kile anachojiapiza hata kwa sababu ndogo. Usifikirie hivyo maishani mwako.

6. NIMEKOSEA KUCHAGUA
Usijihukumu makosa kwa sababu umeona mpenzi wako ana tatizo fulani. Fahamu kuwa kasoro ni sehemu ya ubinadamu. Weka mikakati ya kumuongoza mwezio kuliko kuhitimisha kwa mawazo kwamba ulikosea kumchagua. “Ningejua kama yuko hivi nisingemchagua.” Usiwaze hivi!


7. HATUWEZI KUZAA
Kuna wapenzi ambao kwa kuishi miaka mitatu au minne pamoja bila kupata mtoto hufikia kwenye fikra kwamba hawawezi kuzaa. “Mmm, mwaka wa nne umepita bila mtoto, nadhani sisi hatuwezi kuzaa.” Kwa nini msizae?Hizo ni fikra zako, hamjaambiwa na daktari sasa iweje uwaze hivyo? Jipe moyo kwani kuna watu walizaa baada ya miaka kumi, iweje ninyi wa mwaka mmoja?

8. UNANIDANGANYA
Ipo aina ya watu ambao hata kama wakiambiwa wanapendwa sana, hukimbilia kusema na kuamini kuwa wanadanganywa. “Mmm unanidanganya.” Atasema hivyo licha ya kuona mwanaume anavyojituma kumsotea na kumuonesha kila dalili za mapenzi. Hili ni jambo baya, ukithibitisha kwamba unapendwa usihisi unadanganywa, utapoteza bahati yako.

No comments:

Post a Comment