Tuesday, April 26, 2011

Hasara 5 za ushauri wa rafiki kimapenzi



Watu wengi wamekuwa wepesi sana kukimbilia kwa rafiki zao ili kuomba msaada wa mawazo ya nini wafanye kwenye mapenzi. Imani iliyojengeka kwa watu wengi katika jamii yetu ni kuwa ushauri ni kitu muhimu sana kwa kila hatua.

Kwa mtazamo wa haraka haraka unaweza kuishia kwenye ukomo huo wa fikra na kuamini juu ya ushauri wa mtu kukufikisha mahali sahihi kwenye mapenzi. Unapokerwa na mpenzi unakimbilia kushauriwa na wakati mwingine hata unapotaka kuoa au kuachana na umpendaye, unamuomba rafiki yako ushauri.
Je, umeshawhi kufikiria hasara za kuomba ushauri wa kimapenzi kwa rafiki yako? Hebu ungana nami wiki hii ili nikumegee kidogo hasara za ushauri.

UTAKUPOTOSHA
Ni wazi kwamba kipimo cha uelewa kinatofautiana kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine. Ifahamike kuwa, uhodari wa mambo nao hutofautiana, mtu anaweza kuwa mahiri katika siasa na akaaminika kwenye jamii, lakini ukimpelekea suala la mapenzi anakuwa hajui kitu, hivyo ni rahisi kukupotosha.

Uchunguzi unaonyesha kuwa, wapenzi wengi sana hupotoshwa na rafiki zao wasiokuwa na uelewa wa kutosha juu ya tatizo au suala husika la kimapenzi. Ni vema kuwa makini unaposhauriwa.


UTARAHISISHA MAMBO
Mara nyingi washauri huwa si wao wanaokabiliana na mambo, hivyo ni rahisi kwao kupima vitu kwa juu juu tu na kushauri kirahisi rahisi. “Vipi kakupiga namna hii, aaa huyu si mwanaume kwa kweli ni bora ukaachana naye.” Anasema ni bora kuachana naye kwa sababu haumizwi na kuachana, unayeachana ni wewe anayekushauri.

“Mkubali tu bwana unalaza damu, hiyo tabia yake ya uhuni atabadilika, shosti unataka kuacha bahati ipite?” Kwa mshauri ni rahisi kusema hivyo lakini kumbuka ukubwa wa tatizo hatimaye utakabiliana nao wewe. Hii ina maana kwamba, unapofikiria kuhusu ushauri ufikirie pia kuhusu kushauriwa jambo kirahisi, ukiuvaa mkenge mwenye kuumia utakuwa ni wewe.

UTAKUGEUZA
Ulimwenguni kuna aina zaidi ya 1000 za mapenzi na kila mmoja anatajwa kupenda kwa staili zake. Mapenzi ni kama chembe hai nyekundu zilizopo kwenye damu ya mwanadamu ambazo zinaelezwa na wataalamu kuwa hazifanani hata kidogo. Uzoefu unaonyesha kuwa, washauri wengi hushauri kwa uzoefu wao, lakini je ni sahihi uzoefu huo uwe msaada kwa mtu mwingine?

Jibu ni hapana, kinachotokea mara nyingi kwenye ushauri ni mtu kumfanya mwenzake awe kama yeye alivyo, yaani apuuze aamue na apende kama staili yake, jambo ambalo haliwezekani kabisa kwenye mapenzi. Vipi Juma ageuke ghafla awe kama Hassan kwenye suala la mapenzi? Ushauri ni muhimu lakini upime kama unalingana na matakwa yako.



UTAKUONDOLEA UJASIRI
“Kwa maelezo hayo mumeo ni malaya sana, naona itakuwa vigumu kumbadilisha, ni bora ukaanza maisha yako kwa sababu kuna siku hali itakuwa mbaya.”
Huu ni ushauri ambao unaweza kumuondolea mtu ujasiri wa kukabiliana na tabia ya mumewe hadi kufikia hatua ya kumsaidia akaachana na tabia zake mbaya.

Ushauri huondoa ujasiri wa kukabili tatizo hasa pale anayekushauri atakapolipeleka suala lako kwenye njia ngumu isiyokuwa na ufumbuzi. Ikumbukwe kuwa anayeamini kushindwa ni mshauri lakini wewe kama mwanamke unaweza kusimama kutetea penzi lako na kuliweka sawa mpaka jamii ikasema: “Jamani huyu dada kamrekebisha kweli mumewe, hakuwa hivi alikuwa mlevi lakini sasa kaacha pombe.

UTAKUNYIMA FURSA
Kwenye mapenzi kuna fursa nyingi za mafanikio ambazo unaweza usizipate ukiwa mtu wa kusikiliza sana ushauri wa watu. Kuna wakati ambao unatakiwa usimame wewe kuamua kumpenda mtu ambaye jamii inaona kama utapotea.
Kama somo hili limekufaa niambie kupitia namba hapo juu au tukutane Facebook kwa jina la Richard Manyota, tusemezane zaidi.

No comments:

Post a Comment